Saturday, September 3, 2016

ACACIA YAKABIDHI MADAWATI 2000 SHINYANGA.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO



MGODI wa Dhahabu wa Bulyanhulu,wilayani Kahama,unaomilikiwa na Kampuni ya ACACIA,umekabidhi madawati 2000 yenye thamani ya Shilingi 240,800,000/- yatakayogawiwa katika Shule za Msingi na Sekondari mkoani Shinyanga.

Akizungumza katika hafla fupi ya kukabidhi madawati hayo,iliyofanyika uwanja wa michezo wa Halmashauri ya Mji wa Kahama,Afisa Ufanisi na Ustawi wa Mgodi wa Bulyanhulu,Elias Kasitila, alisema hiyo ni awamu ya nne kukabidhi madawati kwa kipindi cha mwaka 2016,ili kutekeleza kampeni ya serikali  kuhakikisha kila mwanafunzi anaketi kwenye dawati.

Kasitila alisema mbali ya  mgodi huo kukabidhi dawati kwa awamu nne tofauti,umekuwa mstari wa mbele kukichangia  sekta ya elimu Wilaya za Kahama,mkoani Shinyanga na Nyangh’wale mkoani Geita, ikiwemo nyumba za walimu, Maabara, vyumba vya madarasa  na vifaa vya taaluma.

“Tumekuwa tukishirikiana na jamii kutekeleza miradi mbalimbali ya elimu pia mgodi unadhamini masomo kwa wanafunzi,yote hayo lengo likiwa ni kuboresha mazingira ya elimu nchini Tanzania,”alisema Kasitila.

Akipokea madawati hayo kutoka Mgodi wa Dhahabu wa Bulyanhulu, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack,alidai mkoa wake bado unakabiliwa na changamoto kadhaa za kielimu ambazo zimekuwa kichocheo cha kushuka kwa kiwango cha taaluma,zikiwemo kukosekana kwa Nyumba za Walimu na Mabweni ya wanafunzi.

Telack alisema Wilaya za Kahama na Kishapu, bado zinakabiliwa na tatizo kubwa la ukosefu wa nyumba za walimu na mabweni ya wanafunzi kwa shule za sekondari,na kusababisha walimu na wanafunzi kutembea umbali mrefu,kufika shuleni kiasi cha kupunguza ari ya ufundishaji na upokeaji mafunzo.

 “....kuna shule za Msingi katika wilaya hizi,hazina nyumba za walimu,na kuwalazimu walimu kusafiri kila siku kilometa 8 kwenda na kurudi kazini, hali ambayo huwafanya kufika shuleni wamechoka na ufanisi wa kufanya kazi ipasavyo hupungua,”alisema Telack.

 Aidha Mkuu wa Mkoa  huyo alisema katika Wilaya hizo zipo shule za sekondari za Kata,zilizojengwa mbali na makazi,na kulazimu wanafunzi kukimbia kuwahi masomo kwa kusafiri umbali wa kilometa 16 kwenda na kurudi,ambapo hufika wamechoka na kutopokea vizuri masomo wafundishwayo.

Hivyo mkuu huyo wa Mkoa aliwaomba viongozi wa migodi yote ya Bulyanhulu na Buzwagi pamoja na ule wa Almasi uliopo Mkoani Shinyanga kuweka nguvu zaidi kuchangia sekta ya elimu   Wilayani Kahama kwenye shule ambayo haina nyumba za walimu, na   Wilayani Kishapu kwenye sekondari isiyokuwa na mabweni.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI