Sunday, August 21, 2016

MAUAJI YA VIKONGWE YAREJEA KWA KASI WILAYANI KAHAMA.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO



MATUKIO ya mauaji ya vikongwe kwa imani za kishirikina,yameanza kurejea kwa kasi wilayani Kahama,ambapo kwa mwaka huu,vikongwe saba vimeuawa kutokana na imani potofu inayochangiwa na jamii kukosa elimu ya afya inayochangia vifo vya uzembe wa kutowahi matibabu mapema.

Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Kahama,Katibu Tawala wa wilaya ya Kahama, Thimothy Ndanya,alibainisha kwamba katika kipindi cha January hadi Agosti mwaka huu tayari matukio sita ya vikongwe kuuawa kwa imani za kishirikina yametokea,kiwango ambacho amedai ni kikubwa mno kupata kutokea katika wilaya ya Kahama.

Ndanya aliyataja maeneo katika wilaya ya Kahama,ambayo yamekuwa yakitokea matukio hayo ya mauaji mara kwa mara kuwa ni Kata za Kilago katika Halmashauri ya Mji wa Kahama, Chambo na Idahina katika Halmashauri ya Ushetu,huku matukio mawili yaliyosababisa vifo vya watu watatu yakitokea katika Kata mmoja ya Chambo.


Aidha alisema katika tukio lililotokea Agosti 9,mwaka huu la kuuwawa Vikongwe viwili katika Kata ya Chambo,limeshangaza kuona viongozi wanaopewa dhamana ya kuongoza umma nao kuendelea kutawaliwa na fikra za ushirikina,kutokana na  muhusika mkuu kuwa  kiongozi wa serikali ya Kijiji.

“….imeshangaza kuona mwenyekiti wa kijiji hicho ambaye amekimbia na familia yake,kutokuwa kioo cha jamii,kuongoza uhalifu kwa kuwachoma moto vikongwe hao,huku taarifa ya daktari ikionesha mwanae kufariki kwa kutokwa na damu baada ya kujifungua,lakini yeye kuamini vikongwe wale walimroga binti yake,kwakweli suala hili serikali haitalifumbia macho kwani haiko tayari kushuhudia wananchi wake wakiuuawa.”Alisema Ndanya.

Aliikumbusha jamii hasa ya vijijini kuwa na utaratibu wa kupima afya zao mara kwa mara huku ikianzisha mazoea ya kukimbilia katika zahanati ama vituo vya afya pindi wanapougua,kuliko kuchelewa katika matibabu ambayo gharama yake huwa ni vifo ambavyo huwaingiza katika imani za kishirikina.

Kufuatia vifo hivyo vya vikongwe hivyo vilivyofahamika kwa jina moja moja la Mwanabunzali na Mwanazwazwa,Mkuu wa wilaya ya Kahama, Fadhili Nkurlu,ametangaza msako mkali dhidi ya Mwenyekiti wa Kijiji cha Chambo,Clement Shija, pamoja na wenzake waliohusika kuuwa vikongwe hao.

Jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga,linaendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo la mauaji  kwa kuwashikilia watu kadhaa katika Kata hiyo ya Chambo,na jitihada zikiendelea za kuwapata wahusika wengine wakiongozwa na Mwenyekiti huyo ambao wamezikimbia familia zao.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI