Thursday, March 3, 2016

KESI YA KUPINGA UBUNGE,WASIKILIZAJI WASHANGILIA MAHOJIANO MAHAKAMANI.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

 MLALAMIKAJI, James Lembeli, katika Kesi ya kupinga Ushindi wa Mbunge wa Jimbo la Kahama Mjini,Jumanne Kishimba, jana mchana ameeleza Mahakama kuwa alikuwa na uhakika wa kushinda kwa asilimia 95,kama si jitihada za serikali kuupoka ushindi huo.
 
Kauli hiyo imesababisha tafrani kwa muda mahakamani baada ya wasikilizaji waliokuwa wamening’inia katika madirisha ya Mahakama ya Wilaya ya Kahama,kunakofanyika kikao hicho cha Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga,kujikuta wakishangilia kwa nguvu.
 
Katika Mahakama hiyo ambapo kesi hiyo ya kupinga ushindi imeanza kusikilizwa na Jaji Moses Mzuna kutoka jijini Dar Es Salaam,imevuta hisia ya wakazi wa mji wa Kahama wanaojitokeza kusikiliza,lakini wamekuwa wakiathiriwa na udogo wa chumba cha Mahakama,na kusababisha waning’nie madirishani.
 
Mbunge huyo wa zamani wa Jimbo la Kahama,Lembeli akiwa katika mahojiano baina yake na Mwanasheria wa  Serikali, Castuce Ndamugoba,   anasema alikuwa na uhakika wa Ushindi kwa asilimia 95 katika nafasi ya Ubunge wa Jimbo la Kahama Mjini iwapo taratibu za Tume ya Uchaguzi zisingekiukwa na Serikali.
 
Lembeli anasema Serikali ilitumia nguvu na vitisho dhidi ya wafuasi wake na wanachama wa vyama vinavyounda Umoja wa katiba “UKAWA”ambavyo vilikuwa vinamuunga mkono katika Uchaguzi huo.
 
Mwanasheria wa Serikali, Ndamugoba alimtaka Lembeli,aithibitishie mahakama juu ya kauli yake hiyo na vigezo alivyotumia kuamini kuwa alikuwa na uhakika wa ushindi huo.
 
Lembeli alijibu tathimini ya vikao vyake vya ndani baada ya Mikutano ya Kampeni ndivyo vilivyomthibitishia ushindi hususani mikutano yake kuwa na wasikilizaji wengi.
 
Hata hivyo Mwanasheria wa Serikali alihoji ni vipi alitambua wahudhuriaji katika mikutano yake ya Kampeni kama ni wafuasi wa Chadema anaodai kumuunga mkono na hapakuwepo wafuasi wa chama kingine na kwamba waliokuwa wakijaa katika mikutano hiyo walikuwa ni wafuasi wake?
 
Lembeli alisema aliwatambua kutokana na nembo ya chama chake walizokuwa nazo katika uhudhuriaji wa mikutano yake,kuhusu kuwa wafuasi wake alimthibitishia kwa kumueleza atazame umati wa watu uliojazana mahakamani kusikiliza shauri hilo,dalili inayodhihirisha anakubalika.
 
Mwanasheria wa Serikali alihoji kuwa iwapo wafuasi hao waliojitokeza mahakamani hapo ni wafuasi wake?Lembeli hakusita kutamka ni wafuasi wake na kusababisha kuibuka kwa makofi yaliyoambatana na shangwe kutoka kwa wasikilizaji hao na kusababisha Askari Polisi kutoka ndani ya mahakama na kuwatuliza wafuasi hao,ambao baadhi yao walianza kutimka baada ya kubaini wametenda kosa. 
 
 
Lembeli jana alikuwa akitoa maelezo yake binafsi yaliyomfanya afungue kesi hiyo ambayo madai mengine aliyowakilisha mahakamani hapo ni matumizi mabaya ya Serikali wakati wa Uchaguzi,ambapo aliyekuwa Mkurugenzi wa Uchaguzi katika Jimbo la Kahama,alihamishwa akiwa tayari na kiapo cha kusimamia Uchaguzi huo.
 
Madai mengine aliyowakilisha jana ni pamoja na kuhamishwa kwa viongozi wakubwa wa wilaya wakati uchaguzi ukielekea mwishoni,ambao waliohamishwa ni pamoja aliyekuwa Mkuu wa Wilaya hiyo,Benson Mpesya pamoja na Mkuu wa Polisi wa wilaya aliyehamishwa kabla ya siku sita kufanyika kwa Uchaguzi huo.
 
Aidha kufuatia hali hiyo,Lembeli alisema baada ya kuhamishwa kwa viongozi hao,ambao ni wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya,mambo yalianza kubadilika ikiwa ni pamoja na kukamatwa hovyo kwa wafuasi wake wakiwemo mawakala wake walikamatwa na Polisi siku ya kuamkia Uchaguzi.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI