Thursday, February 11, 2016

KAHAMA WARIDHIA ISAKA KUWA MAMLAKA YA MJI MDOGO.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

DIWANI Kata ya Isaka.
BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Msalala,wilayani Kahama,limeridhia kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Isaka,ili kusogeza huduma kwa wananchi na kusaidia kuboresha mapato yatakayosaidia kupatikana maendeleo stahiki na kwa wakati sambamba na kukuza uchumi wa Taifa.
 
Akiwasilisha mapendekezo hayo katika Kikao cha Kawaida cha Baraza hilo,Mkurugenzi wa Halmashauri ya Msalala,Patrick Kalangwa,alisema walipokea mapendekezo ya kuanzishwa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Isaka kutoka Kata ya Isaka kwa barua iliyowasilishwa ofisini mwake Januari 4,mwaka huu.
 
Kalangwa alisema kimsingi mapendekezo hayo baada ya kupitiwa na wataalamu yalionekana yana tija kwa maslahi ya Taifa na wananchi wa maeneo hayo,hasa kwakuwa itasaidia kuboresha ukusanyaji wa mapato utakaosaidia upatikanaji maendeleo kwa wakati katika eneo hilo na kukuza uchumi wa wananchi na Taifa.
 
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Isaka,Dr.Gereld Mwanzia,alisema kutokana na ukubwa wa mji,rasiliamali na miundo mbinu  iliyopo huku tangu mwaka 1994 ukitangazwa na gazeti la serikali kuwa eneo la mipango miji,ni vyema ukawa Mamlaka wa Mji Mdogo.
 
Dr.Mwanzia alisema Kata hiyo   ina wakazi 15,928 wakiwemo wafanyabiashara wanaomiliki maduka ya jumla sita,rejareja 152  ,nyumba za kulala wageni 124,pia kuna ofisi za serikali nane,za Uhamiaji,Polisi,TRA,TTCL,TRL,Bandari ya Nchi kavu na Mahakama sambamba na uwepo wa makampuni makubwa 34 yanayojihusisha na usafirishaji na ujenzi.
 
Madiwani hao kwa kauli moja waliridhia uanzishwaji wa Mamlaka hiyo na kuanisha Kata za Isaka,Mwanase,Mwakata,Mwaluguru na Janna kuunda Mamlaka hiyo huku wakipendekeza Kata ya Isaka ndiyo kuwa makao makuu yake kutokana na miundo mbinu yake ikiwemo kuwepo kwa ofisi za serikali na makampuni.
 
Halmashauri ya Msalala ni kati ya Halmashauri tatu zinazounda wilaya ya Kahama,ambayo ni kubwa kwa eneo hivyo kusababisha baadhi ya wananchi wa Kata za pemebezoni kuchelewa kupata huduma mbalimbali za kijamii.
 

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI