Tuesday, December 16, 2014

UCHAGUZI KAHAMA WATAWALIWA NA DOSARI

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

UCHAGUZI  wa Serikali  za Mitaa uliofanyika Jumapili iliyopita na kutawaliwa na dosari mbalimbali nchini,wilayani Kahama mbali ya kutokea matukio ya kupigwa mabomu ya machozi na kujeruhiwa kwa baadhi ya wasimamizi wa upigaji kura imelazimika kwa baadhi ya vituo kurudia uchaguzi.


Katika Halmashauri ya Mji wa Kahama,ambapo mchuano mkali ulikuwa baina ya Chama Cha Mapinduzi “CCM”na Chama cha Demokrasia na Maendeleo “CHADEMA”,Chama tawala kimeshindwa kutetea viti vyake vingi.

Akizungumza na Waandishi wa Habari ofisini mwake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Kahama;Felix Kimario,alisema uchaguzi huo uligawanyika  katika maeneo matatu;ya Serikali za Mitaa,Vijiji na Vitongoji.

“Unajua maeneo ya pembezoni mwa Halmashauri hii bado yana hadhi ya vijiji hivyo ndio maana upo uchaguzi huo,ambapo tuna vijiji 45,lakini kwa upande wa Serikali ya mitaa kuna mitaa 32,na vitongoji 218,”Alisema Kimario.

Kimario alisema  katika Uchaguzi wa mitaa,Chadema imepata mitaa 15 huku CCM ikipata mitaa 14, ya Igalilimi,Namanga pamoja na Seeke ambao walipita bila kupingwa,huku CCM ikiongoza katika ushindi  wa Wenyeviti wa Vijiji 40 na Chadema  ikipata viti vitano.

Kwa upande wa Vitongoji 218,CCM tayari ina mtaji wa vitongoji 69 waliopita bila kupingwa,huku vitongoji 149 vikiwa vikihakikiwa kura zake kabla ya kutangazwa washindi.

Aidha Mkurugenzi huyo alisema katika vituo vya Mhongolo  na Mbulu,uchaguzi ulivurugika baada ya kuzuka vurugu za wapiga kura na kusababisha wasimamizi wawili kujeruhiwa sambamba na  kuharibu pikipiki ya mmoja wa wasimamizi hao,majeruhi hao walipatiwa matibabu katika hospitali ya mji wa Kahama.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ushetu,Isabela Chilumba alisema katika kata 20 zilizopo kata nne za Kinamapula,Ushetu,Ukune na Chona kuna vituo ambavyo uchaguzi haukuweza kufanyika kutokana na dosari zilizojitokeza zikiwemo za wagombea kura zao kugongana.

Alivitaja vituo hivyo kuwa ni Vijiji vya Hongwa na Butibu katika Kata ya Kinamapula,Vitongoji vya Katule B na Italike Mashariki vilivyo Kata ya Ukune,pia Kitongoji cha Nsimbo kata ya Ushetu na Kitongoji cha Usiulize kata ya Chona.Katika Kata ambazo uchaguzi ulikamilika kura zilikuwa bado zinahakikiwa kabla ya kutangazwa kwa washindi.

Nae Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala alisema ni kata sita tu ndizo zilizokamilisha uchaguzi kati ya kata 18 zilizo katika Halmashauri yake,ambapo ameomba radhi kwa wananchi ambao Kata zao hazikuweza kufanya Uchaguzi kutokana na dosari mbalimbali zilizojitokeza ikwemo kuchelewa kufika kwa wakati kwa vifaa vya kupigia kura.

Alizitaja Kata ambazo hazikuweza kufanya uchaguzi kuwa ni Isaka,Bulyanhulu,Ngaya,Ntobo ,Bugarama,Ikinda,Bulige,Segese,Mwalugulu,Mega,Mwakata na Kashishi.


KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI