Wednesday, May 11, 2016

MILIONI 216 KUANZISHA MFUKO WA MAENDELEO KATA YA ISAKA;KAHAMA.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

WAKAZI wa Kata ya Isaka,katika Halmashauri ya Msalala,wilayani Kahama,wameazimia kuchanga zaidi ya Shilingi 216 Milioni,kwa ajili ya kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Kata,utakaotatua changamoto zinazoikabili Kata hiyo katika sekta ya Afya na Elimu.
Akizungumza katika Mkutano wa Hadhara,Diwani wa Kata ya Isaka,Dk.Gerald Mwanzia,aliwahamasisha wananchi kuona umuhimu wa kuchanga fedha hizo kwa ajili ya kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya tano katika kuleta maendeleo.
Dk.Mwanzia alisema pamoja na mikakati mizuri ya Serikali katika kuhakikisha nchi inapiga hatua katika maendeleo,ni budi wananchi kutobweteka kwa kujitoa kuchangia na kuchangia nguvu zao hatua itakayowezesha kupiga hatua kubwa ya maendeleo.
“Tuna changamoto kubwa katika Kata yetu,lakini ni vyema tuweke vipaumbele vya elimu na afya,tujitoe kwa moyo mmoja kuchanga kwa hiari fedha ili kuboresha miundo mbinu katika sekta hizo,ndipo tuipigie kelele serikali kuu kutuongezea nguvu,”alisema Dk.Mwanzia.
Alisema  kutokana na Kata hiyo kukabiliwa na changamoto za Afya na Elimu,Kamati ya Maendeleo ya Kata ilifanya utafiti kisha kuafikiana ni budi kutengeneza mpango mkakati wa maendeleo ambao ni kuanzisha Mfuko huo ili kukabiliana na tatizo hilo,kwa kupendekeza kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi achange kiasi cha Shilingi Elfu 36 kwa miaka mitatu.
Aidha alisema Kata hiyo ambayo ina wakazi 6000 wenye uwezo wa kufanya kazi,kila mmoja atawajibika kuchanga Shilingi Elfu 12 kwa mwaka,huku ukiandaliwa mpango madhubuti wa kuwafikia wadau wa maendeleo waliopo  katika Kata hiyo kama makampuni na mashirika ili kutunisha mfuko huo.

Alifafanua Mfuko huo utasaidia kuboresha miundo mbinu ya Shule za Msingi na Sekondari,na kutengeneza mazingira bora ya kujifunzia kwa wanafunzi na kufundishia kwa walimu hivyo kuleta chachu ya ufaulu mzuri kwa vijana, sambamba na kuboresha Kituo cha Afya na zahanati ili kuleta ufanisi bora wa huduma hiyo.
Wanachi waliojitokea katika mikutano hiyo ya kuhamasisha uanzishwaji wa Mfuko huo wa maendeleo,walipongeza mpango huo kwa kuwa unagharama nafuu kwa mwananchi,hivyo hawaoni sababu ya jamii kutochangia mkakati huo.
“Ningeomba tuupokee mpango huu wa Diwani na Kamati yake ya Maendeleo ya Kata,kwa mustakabari wa sekta za elimu na Afya,tutambue kila mtu anapenda raha,pindi vijana wetu wakifanya vyema katika masomo ni faraja kwetu na hili linawezekana pindi miundo mbinu ikiboreshwa,”alisema Salum Kulindwa.
Katika sekta ya Elimu Kata ya Isaka inakabiliwa na upungufu wa madarasa 37,madawati 321 na matundu ya vyoo 105 kwa shule za msingi huku zikiwa hazina ofisi wala maktaba,huku mfuko huo ukiwa na lengo la kuondoa changamoto hiyo kwa kipindi cha miaka mitatu sambamba na kuipandisha hadhi Kituo chao cha Afya huku Sekondari yao wakitaka iwe na Kidato cha tano na sita.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI