Friday, April 8, 2016

RAIS MAGUFULI MGENI RASMI MAADHIMISHO YA MEI MOSI.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO



RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,John Pombe Magufuli, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya sherehe ya Siku ya Wafanyakazi Duniani,“Mei Mosi” ambayo mwaka huu kitaifa yatafanyika,Makao Makuu ya Nchi,Dodoma.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Nicholas Mgaya, wakati  jana alipokuwa na Kamati yake ya maandalizi ya maadhimisho hayo katika kikao chao kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Jordan Rugimbana,alisema Rais Magufuli atahudhuria maadhimisho hayo kwa mara ya kwanza akiwa na wadhifa wa ukuu wa nchi.

Mgaya alisema Tucta waliwasilisha maombi rasmi ya kumuomba Rais Magufuli kuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho hayo na tayari wamepata taarifa rasmi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kuwa Rais amekubali kuwa mgeni rasmi.

Katika kikao hicho ambacho kilikuwa na lengo la kujadili na kuendelea kuweka mipango na maandalizi ya kufanikisha sherehe za mwaka huu kwa mafanikio makubwa,Mgaya alisema ni faraja kwa Mkuu huyo wa Nchi kukubali kushiriki katika Maadhimisho hayo ambayo pia yanafanyika Makao Makuu ya Nchi.

Alisema ili kufanikisha sherehe za Mei Mosi, Tucta Makao makuu watachangia nusu ya gharama zote za sherehe nzima na nusu inayobaki itachangiwa na wadau mbalimbali wakiwemo waajiri ambapo kwa mujibu wa Kamati ya Maandalizi Bajeti nzima ya sherehe ya mwaka huu ni Sh milioni 29.6.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa Rugimbana aliishukuru Tucta na Serikali kwa ujumla kwa kuupa Mkoa wa Dodoma ambao ni Makao Makuu ya Nchi heshima ya kipekee ya kuwa mwenyeji wa maadhimisho ya sherehe ya Sikukuu ya Mei Mosi Kitaifa mwaka huu.

Naye Katibu wa Tucta Mkoa wa Dodoma, Ramadhani Mwendwa alisema tayari wameunda kamati ya maandalizi ya sherehe na jukumu kubwa lililoko mbele ni kutafuta fedha na michango kutoka kwa wadau, wengi wao wakiwa ni waajiri serikalini.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI