Thursday, April 28, 2016

MADIWANI,MBUNGE KAHAMA WAPINGANA KUHUSU MIUNDO MBINU.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

BARAZA la madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kahama, limeikataa taarifa ya utekelezaji wa miundombinu ya barabara kutokana na kutopita katika kamati husika, na kuzua marumbano baina yao na mbunge wa Jimbo la Kahama,Jumanne Kishimba,aliyetaka ijadiliwe ili kuibua ufisadi katika Halmashauri hiyo.
 
Katika kikao maalumu cha Baraza hilo,madiwani walipinga kuwasilishwa kwa taarifa hiyo,ambapo Mwenyekiti wa Kamati ya Mpango Mji na Mazingira, Bernad Mahongo, alisema wanaitilia shaka taarifa hiyo kutokana na kutopitia katika kamati yake kujadiliwa kabla ya kufikishwa mbele ya Baraza la madiwani.
 
 Mahongo ambaye pia ni diwani wa kata ya Majengo alisema taarifa hiyo haijawahi kujadiliwa na kamati yake na kwamba irudishwe ili iweze kujadiliwa upya,kwa mujibu wa kanuni za Halmashauri zinavyoelekeza.  
 
Hata hivyo Mbunge wa Jimbo la Kahama,Jumanne Kishimba,alidai kutopita katika Kamati husika kwa hoja hiyo ni muendelezo wa ubadhirifu na ufisadi uliokithiri kwa wataalamu na watendaji wa Halmashauri hiyo hivyo kupendekeza waijadili ili kuibua madudu,ambayo walilenga kuyafanya,jambo ambalo lilipingwa na madiwani kwa kusisitiza irudi katika Kamati Husika.
 
Kufuatia hoja hiyo iliyoibua hofu ya wizi na matumizi mabaya ya fedha katika taarifa ya miundombinu ya bara bara, mhandisi wa mji, Eng Job Mutagwaba, alisema suala la miundombinu haswa ya bara bara inahitaji utaalamu mkubwa,na kama madiwani wanahofu na utendaji kazi wao wapo tayari kuchunguzwa na Takukuru.
 
Hata hivyo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kahama, Anderson Msumba, alifafanua taarifa hiyo iliwasilishwa kimakosa sambamba na kutokuwa sahihi kutokana na kuwa ni  taarifa   ya utekelezaji wa miundombinu ya mwaka 2014/15 na kwamba ilishafanyika na ikalipwa.
     
“Taarifa hii Mkuu wa Idara amejichanganya,iliishafanyika na tayari imelipwa,nawaomba radhi, nakuahidini  hali hii haitojirudia tena,”alisema Msumba. 
 
 Madiwani wa halmashauri ya mji wa kahama walikutana kujadili taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbali mbali za miradi ya maendeleo kwa robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2015/016.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI