Friday, December 18, 2015

MADIWANI KAHAMA WAMKATAA MAKAMBA,NAE ATISHIA KUFICHUA UFISADI.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

MADIWANI katika Halmashauri ya Mji wa Kahama{CCM}wamepinga Mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Shinyanga,Salome Makamba{CHADEMA}, kupangwa katika Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri hiyo,huku naye akiwaonya Madiwani kuwa atahakikisha anatumbua majipu pindi wakiendeleza matumizi mabovu ya fedha za Maendeleo.
 
Hali hiyo iliibuka juzi katika kikao cha kwanza cha Baraza la pili la Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kahama lenye Madiwani 29,ambapo kutoka upinzani wapo madiwani wawili tu,kilichokuwa cha kuapishwa,kuchagua Mwenyekiti na kupanga Kamati mbalimbali ndipo Madiwani hao wa CCM walipoungana kupinga Mbunge huyo kupangwa Kamati ya Fedha ya Halmashauri hiyo.
 
Diwani wa viti Maalumu,Aoko Nyangusu{CCM} alihoji kanuni iliyotumika kumuingiza mbunge huyo kwenye kamati ya fedha,wakati wabunge wa viti maalumu hawahusishwi katika Halmashauri zao,mara Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji,Abeli Shija,alipomaliza kuwatangaza wajumbe wake,huku jina la Makamba likiwemo.
 
Hoja iliyoungwa mkono na Madiwani wote watokanao na CCM,huku Diwani wa Kata ya Mhongolo,Michael Mizubo,akisoma muongozo wa Halmashauri ambao unamtaja Mbunge wa Jimbo kuwa mjumbe katika Kamati hiyo,ndipo Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo,Anderson Msumba,alipotoa ufafanuzi kipengere kilichotumika kilifanyiwa marekebisho Bunge lililopita.
 
“Waheshimiwa kumbukeni tunaongozwa na Katiba,Sheria za Bunge na Muongozo wa Halmashauri,vyote tumezingatia katika kumpanga Mbunge huyo,mtambue katika maelekezo ya sasa lazima awemo diwani wa kutoka vyama vya upinzani,na kwa kuwa hakuna madiwani wengi wa upinzani na mheshimiwa Makamba anatoka chama cha upinzani hivyo yuko sahihi kuwemo kwenye kamati hiyo” alisema Mkurugenzi huyo
 
Hata hivyo madiwani hao hawakuridhika na majibu hayo huku wakitaka jina la Makamba liondolewe miongoni mwa wajumbe wa Kamati hiyo,na kumlazimu Mbunge wa jimbo la Kahama,Jumanne Kishimba,kunyanyuka na kuhoji sababu ya kumkataa Makamba kama kweli wanadhamira ya kuwatumikia wananchi kuleta maendeleo,huku akitia shaka kuwa huenda kuna chembe za ufisadi unaowatia hofu wajumbe ambao walikuwemo katika Baraza la Madiwani lililopita.
 
Kwa upande wake Mbunge wa Viti Maalumu,Makamba{CHADEMA},alishangazwa na misimamo hiyo ya madiwani na kuhoji katika kamati hiyo kuna nini hadi kumgomea asiwemo,aliwahakikishia kuwa atasimamia maslahi ya Kahama na Taifa kwa ujumla kwa kufichua ubadhirifu wa fedha za maendeleo hata akiwa nje ya ukumbi mbali ya kutokuwemo katika Kamati hiyo.
 
Nimeshangazwa na kitendo cha kugoma nisiingie kwenye Kamati ya Fedha na Mipango,hapa kuna kitu huenda mna maslahi yenu binafsi,lakini naahidi   hata mkinikataa nitafanya kazi ya kamati hiyo nikiwa nje ya kikao,na kwa kuanza napenda Halmashauri inapatie mchanganuo wa matumizi ya fedha za mrabaha wa Mgodi wa Dhahabu wa Buzwagi kwa miaka iliyopita,ambako mimi nilikuwa mtumishi,maana natambua kuna madudu yamefanyika katika fedha hizo” alisema Makamba
 
Malumbano katika Baraza hilo lenye Madiwani wa Kata 20,viti maalumu saba na wabunge wawili,yalihitimishwa kwa Mkurugenzi kuwaahidi kuwapatia waraka ambao umefafanua juu ya uendeshaji wa Halmashauri,ambao unazingatia Katiba ya nchi,Sheria na muongozo wa Halmashauri kuwa ni wa tatu,ambao hauwezi kukiuka na kuvunja maamuzi ya vikao vya Bunge.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI