Saturday, November 28, 2015

HALMASHAURI ZASHUTUMIWA KUZORETESHA KILIMO CHA ZAO LA PAMBA WILAYANI KAHAMA.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

 
 
 HALMASHAURI za Ushetu na Msalala,zimeshutumiwa kuchangia kuzorota kwa kilimo cha zao la Pamba katika wilaya ya Kahama,kutokana na kuchukua ushuru huku wakishindwa kuboresha miundo mbinu ya barabara kuelekea vijiji vinavyolima zao hilo.
 
Shutuma hizo zilitolewa na Chama cha Wakulima  wa zao la Pamba Tanzania“TACOGA”Tawi la Kahama,ambapo kilisema katika kipindi hiki cha masika miundo mingi ya barabara imeharibika na kutopitika,hivyo kusababisha pembejeo za zao hilo kutofikishwa kwa wakati.
 
Akiongea na Tanzania Daima,Katibu wa Tacoga wilaya ya Kahama,Paul Ntelya,alisema suala la miundo mbinu ya barabara kuwa mibovu,nayo inachangia kuzorota kwa zao hilo wilayani Kahama,kutokana pembejeo kutofika kwa wakati katika kipindi hiki ambacho barabara zimeharibiwa na mvua.
 
“Mvua zimeharibu barabara,baadhi ya makampuni ya wanunuzi wa zao la Pamba,walipeleka mbegu kwa wakulima,lakini gari zao zimezama kabla hazijaenda kituo kingine kupeleka mbegu,msimu wa masika nao hausimami matokeo yake watapanda kipindi kimepita matokeo yake ni kutopata tija katika zao hilo,”alisema Ntelya.
 
Alisema Halmashauri hizo zimekuwa mstari wa mbele kuchukua ushuru wa zao hilo huku ikishindwa kuboresha miundo mbinu hiyo ambayo ni muhimu kwa usafirishaji wa pembejeo na zao hilo kulifikisha sokoni kwa wakati kitendo ambacho hakiwatendei haki wakulima na kuwafanya kukata tamaa ya kuzalisha zao hilo kwa wingi.
 
Aidha Katibu huyo alitoa ushauri kwa Serikali kufuta ushuru huo na kuongeza katika Bei ya zao la pamba ili mkulima anufaike jambo litakalomtia hamasa zaidi katika kuboresha kilimo chake huku akihamasika kuchangia  shughuli mbalimbali za  miradi ya maendeleo inayoibuliwa na wananchi wenyewe katika vijiji vyao ikiwemo ujenzi bora wa barabara.
 
Katika hatua nyingine Mbunge wa Jimbo la Ushetu,Elias Kwandikwa,aliwataka wakandarasi wote watakaopewa na Halmashauri kwa ajili ya kufanya kazi katika jimbo analoongoza kuhakikisha wanaweka wazi mikataba yao kwa wananchi sambamba  na kuonesha mpango kazi wao unapoanzia na unapoishia,ili kuondoa walakini kwa wananchi.
 
Kwandikwa alisema hatua hiyo itasaidia ujenzi imara wa miundo mbinu itakayokuwa na tija kwa wakulima wa maeneo ya vijijini na hivyo kusaidia kuinua kipato cha mkulima kwa kupata pemebejeo na kuuza mazao kwa wakati na kusaidia kuinua uchumi wa nchi.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI