Thursday, July 21, 2016

UJASIRIAMALI KUONDOA MIGOGORO NA MWEKEZAJI

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO


IMEELEZWA kwamba kuanzishwa kwa vikundi vya vijana katika eneo linalozunguka Migodi kisha kupatiwa elimu ya ujasiriamali,itasaidia kuondoa migogoro baina ya Mwekezaji na jamii ambayo itakuwa imepatiwa elimu ya kujikwamua kiuchumi kupitia fursa mbalimbali za Ujasiriamali.
 
Hayo yalielezwa na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nyang’hwale, Venance Ngereuya,wakati wa ufungaji mkataba baina ya Mgodi wa Bulyanhulu uliopo Wilayani Kahama na Shirika lisilo la Kiserikali la Africare,unaogharimu Shilingi milioni 600.
 
Mkataba huo huo utakaodumu kwa kipindi cha mwaka mmoja na nusu ni  kwa ajili ya kuunda vikundi vya ujasiliamali kwa vijana waishio kuzunguka migodi huo,utawanufaisha vijana kutoka vijiji viwili  katika Wilaya za Nyang’hwale mkoani Geita  na vingine 12 kutoka Halmashauri ya Msalala Wilayani Kahama
 
Ngereuya alisema uanzishwaji wa vikundi hivyo vya vijana kupitia mradi utakaotekelezwa na Africare,utasaidia kuondoa dhana ya vijana kuwa ajira ni budi ufanye kazi Mgodini,bali ujasiriamali utaweza kuwakwamua kimaisha kwa kutumia fursa zitakazowawezesha kufanya biashara na Mwekezaji.
 
Hata hivyo aliomba uanzishwaji wa vikundi hivyo sambamba na utoaji elimu,ufanyike kwa umakini mkubwa kwa kulenga vijana stahiki kutoka katika vijiji husika,vinginevyo tatizo la ajira katika maeneo hayo halitatuliwa pindi wakinufaika vijana ambao hawana maslahi na vijiji hivyo.
 
“Kama umakini usipotumika kupata vijana sahihi katika maeneo hayo,vijiji hivyo havitanufaika na tatizo tutakuwa hatujaliondoa,kwani iwapo elimu itawafikia vijana wasio na asili ya maeneo husika wataondoka wakinufaika na mafunzo hayo kwenda kuyatumia walikotoka,”alisema Ngereuya.
 
Kwa upande wake Meneja Ustawi na Ufanisi wa Mgodi,Elias Kasitila,alisema mradi huo utakaotekelezwa na Africare umefika kwa wakati muafaka,kwani utatoa fursa kwa vijana ambao wamehamia katika eneo la Mgodi kwa lengo la kutafuta ajira,kutambua kuna fursa za kujiajiri na kufanya biashara na Mgodi na si kutegemea kuajiriwa.
 
 
Kasitila alisema mpango huo ambao utatekelezwa kwa ushirikiano wa pande tatu ambazo ni mgodi wake wa Bulyanhulu, shirika la Africare Tanzania pamoja na serikali katika Halmashauri hizo mbili za Nyang’hwale na Msalala ambazo zitatoa wataalamukwa ajili ya ushauri na kusimamia mpango huo.
 
Kwa upande wake,Kaimu Mkurugenzi wa shirika la Africare Tanzania, Alfred Kalaghe, alisema kupitia mradi huo wa miradi midogomidogo ya kuboresha Uchumi,utaanza kutoa mafunzo kwa vijana kabla ya kuunda vikundi vitakavyowezeshwa mitaji ya kufanya biashara,na watajikita kwenye nyanja mbalimbali ikiwemo kilimo na ufugaji.
 
“.... vijana hao tutawawezesha kilimo cha kisasa ambacho kitazalisha mazao bora yatakayosimama, kwenye masoko na kusaidia kuwainua kiuchumi,na kuondokana na ndoto za kukimbilia kwenye machimbo kusaka ajira,”alisema Kalaghe.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI