Utafiti
uliofanyika hivi karibuni na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) umebaini kwamba
asilimia 71 ya watanzania wanatumia muda mwingi kufanya shughuli zisizokuwa za
uzalishaji mali wala tija binafsi kwao na Taifa kwa ujumla.
Akizundua
taarifa ya utafiti huo leo jijini Dar es salaam Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu Sera,Bunge,Kazi,Ajira,Vijana na watu wenye ulemavu Mhe. Jenista
Mhagama amesema kuwa idadi hiyo hufanya kazi zisizoleta tija kwao na
taifa na muda mwingi huutumia kujihudumia binafsi kwa kulala na starehe
nyingine.
Ameeleza
kuwa takwimu hizo zinaonesha wazi ni kwa namna gani watanzania wanashindwa
kujishughulisha katika kufanya kazi zenye kuwaingizia kipato na badala yake
wanatumia muda wao mwingi kufanya shughuli zisizo za uzalishaji hasa kufanya
starehe mbalimbali.
“
Ndugu zangu watanzania unakuta mtu amekaa baa au anacheza “poll table” kuanzia
asubuhi mpaka jioni na hujui anafanya kazi gani ya uzalishaji, ndugu zangu
tuone aibu basi tujishugulishe tulijenge taifa letu ili kujiletea maendeleo
yetu na nchi yetu.”
Aidha,
matokeo hayo yamebainisha kuwa asilimia 18.5 ya wananchi wanafanya kazi za
uzalishaji na asilimia 10.6 ni wale wanaofanya shughuli za nyumbani zisizo na
malipo huku uchambuzi wa kijinsia ukionesha kuwa wanaume asilimia 23.8,
wanatumia muda mwingi kwenye shughuli za kiuchumi ikilinganishwa na asilimia
13.5 ya wanawake.
![]() |
Waziri
wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,Bunge,Kazi,Vijana,Ajira na Wenye
Ulemavu),Jenista Mhagama,akizindua ripoti ya matokeo ya utafiti wa watu wenye
uwezo wa kufanya kazi wa mwaka 2014
|
Amefafanua
kuwa wanawake ambao ni asilimia 16.5 katika utafiti huo wanatumia muda mwingi
kufanya kazi za nyumbani zisizo na malipo ikilinganishwa na asilimia 4.4 ya
wanaume.
Utafiti
huo ulibaini asilimia hiyo ni ya
Watanzania wenye umri kuanzia miaka 15 hadi 35,ambao wanatumia muda wao mwingi kwenye shughuli
zisizo za uzalishaji mali.
Katika utafiti huo imefahamika Badala ya kutumia muda huo katika shughuli za uzalishaji mali huutumia kujihudumia kwenye gesti, baa, kulala na katika shughuli za starehe.
Serikali imesema hali hii inaichelewesha Tanzania kuingia katika kundi la mataifa yenye uchumi wa kati kufikia mwaka 2025.
Bi Ruth Minja, ambaye ni mtakwimu mkuu katika ofisi ya taifa ya takwimu Tanzania, ndiye aliyeongoza utafiti huo wa watu wenye uwezo wa kufanya kazi kwa mwaka 2014/2015.
Anasema
waligundua kuwa watu wenye uwezo wa kufanya kazi walikuwa milioni 25 kutokana
na kiashiria cha saa za kufanya kazi kupungua na baadhi ya wafanyakazi
kupunguzwa kazi kutokana na utendaji dhaifu.
Aidha
Ally Msaki, aliyemuwakilisha Katibu Mkuu katika Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia
masuala ya kazi,vijana ajira na watu wenye ulemavu , amewaangazia Watanzania
walioko kwenye ajira, ambao wanapata kipato ambacho hakitoshelezi kuweza kumudu
gharama za maisha.
Amesema nafasi kama hizo za kazi hazina viwango vya ubora na ni kinyume cha maelekezo ya shirika la wafanya kazi duniani ILO.
Ingawa Sera ya taifa ya ajira kwa Taifa la Tanzania kwa mwaka 2008 ilijikita zaidi katika kuongeza fursa za ajira na kufanikiwa katika lengo lake, kuna kasoro kwenye kipengele cha ubora wa ajira
Kwa
upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Ofisa ya Taifa ya Takwimu (NBS) Dkt. Albina
Chuwa amesema kuwa upatikanaji wa Takwimu hizo utaisaidia Serikali kupata mbinu
sahihi za kuondokana na tatizo la ajira nchini kwa kuunganisha nguvu kutoka
sekta isiyo rasmi ili kuleta changamoto katika soko la ajira nchini.
Amesema
kuwa hii ni mara ya tano Tanzania inafanya utafiti huo na kubainisha kuwa
ulianza mwezi Januari hadi Desemba, 2015 ukitumia sampuli ya
Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 iliyotumika kupata taarifa sahihi
ya takwimu hizo.
Aidha,
amebainisha kuwa ili kufanikisha utafiti huo NBS imeshirikiana na wadau
mbalimbali ikwemo Wizara ya kazi na Ajira,Shirika la Kazi Duniani (ILO),Benki
ya Dunia (WB),Benki ya Maendeleo ya Afrika(ADB) na Asasi zisizo za Kiseikali.