Friday, August 21, 2026

RAIS SAMIA APONGEZWA KWA KUTOA FURSA ZA UWEKEZAJI NA AJIRA KWA VIJANA.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO

 

RAIS SAMIA APONGEZWA KWA KUTOA         FURSA ZA UWEKEZAJI NA AJIRA KWA VIJANA.                            

 


Na Ali Lityawi, Kahama.

 

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongezwa kwa kuendelea kuweka mazingira yanayowawezesha wawekezaji wazawa kuwekeza, hatua inayoongeza ajira na kuchangia ukuaji wa uchumi nchini.

 

Meneja wa Kituo cha Mafuta cha Ngara Oil, Nuru Christopher Nzoya, alisema hayo mbele ya Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Michael Mwang'onda, Kahama, Shinyanga.

 


Nzoya alisema fursa zinazotolewa na Serikali zimewezesha wawekezaji wazawa kuanzisha miradi, hatua inayotarajiwa kutoa ajira kwa vijana wengi wasiokuwa na ajira nchini.

 

Alisema uwekezaji huo utasaidia vijana kujikimu kimaisha, huku ukichangia pia kukuza uchumi wa Taifa kupitia shughuli za biashara na ongezeko la fursa mbalimbali.

 


Nzoya alisema ujenzi wa kituo hicho ulianza Januari saba mwaka huu, na unatarajiwa kukamilika Oktoba 30, mwaka huu, kwa mujibu wa mipango iliyowekwa.

 

Alisema mradi huo unalenga kutekeleza sera ya Serikali ya kuwashirikisha wadau wa ndani katika uwekezaji wa sekta mbalimbali, kukuza uchumi na kuongeza ajira nchini.

 


Alibainisha kuwa kituo hicho kitakapokamilika na kuanza kutoa huduma za mafuta, kinatarajiwa kutoa ajira kwa watumishi 20 katika Manispaa ya Kahama.

 

Kwa mujibu wa Nzoya, mradi huo hadi kukamilika kwake utagharimu Shilingi milioni 821.5, huku ukiwa na matarajio ya kuongeza shughuli za kiuchumi eneo hilo.

 


Akizungumza baada ya kutembelea kituo hicho na kujiridhisha, Mwang'onda alimpongeza mwekezaji mzawa kwa kuanzisha mradi mkubwa wenye matarajio makubwa ya kuleta tija eneo husika.

 


Mwang'onda aliwashauri viongozi wa Halmashauri zote nchini kuweka mazingira mazuri ya miundombinu ili kuwawezesha wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza.

 

Alisema mazingira rafiki kwa wawekezaji ni sehemu ya utekelezaji wa sera ya Taifa inayolenga kuwashirikisha wadau katika uwekezaji wa sekta mbalimbali za biashara nchini.

 




Aliongeza kuwa uwekezaji unaochochewa na mazingira mazuri utasaidia kukuza uchumi, kuongeza ajira kwa vijana na kuwawezesha wananchi kujikimu kimaisha.

 


KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI