KAHAMA
YAVUKA LENGO LA USAJILI NeST KWA ASILIMIA 217.
Na Ali
Lityawi, Kahama
HALMASHAURI
ya Manispaa ya Kahama imevuka lengo la kitaifa la usajili wa makundi maalum
kwenye Mfumo wa Manunuzi ya Umma kwa njia ya Kielektroniki (NeST), baada ya
kusajili vikundi 326 kati ya 150 vilivyolengwa.
Kufuatia
mafanikio hayo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Wazo Mwang’onda,
amempongeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Masudi Kibetu, kwa kusimamia
utekelezaji uliofanikisha usajili huo kwa asilimia 217.
Mwang’onda
alitoa pongezi hizo baada ya kupokea taarifa katika banda la Mamlaka ya
Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), lililopo viwanja vya Stendi Ndogo ya
Malori, Kata ya Majengo, wakati wa ziara yake Kahama.
Alisema
kuvuka zaidi ya mara mbili ya lengo lililowekwa ni ishara ya uongozi bora, hasa
katika kuhakikisha vijana, wanawake na makundi mengine maalum yanapata fursa za
kunufaika na fedha za serikali kupitia zabuni.
Awali,
Afisa Maendeleo ya Jamii wa Manispaa ya Kahama, Mbwana Karata, alisema hadi
Agosti 15 mwaka huu, vikundi 326 vilikuwa vimesajiliwa, vikijumuisha vikundi vya
vijana 173, vya wanawake 150, vya watu wenye ulemavu viwili na wazee kikundi
mmoja.
Karata
alisema halmashauri imetenga zabuni zenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 1.9,
huku vikundi vinne vikiwa tayari vimetunukiwa zabuni zenye thamani ya Sh
milioni 242.45.


