NI Mshangao uliochanganyikana na
Simanzi,kufuatia Kifo cha ghafla,kilichoaacha majonzi kwa ndugu,jamaa na
marafiki,cha Jacob Paul ( 36 )mkazi wa Manispaa ya
Shinyanga,kilichotokana na
kujinyonga.
Ni taarifa ambazo zimewafanya Mamia ya
wakazi wa Shinyanga kupigwa butwaa baada ya Jacob Paul,ambaye ni Mwenyekiti wa
chama cha waendesha pikipiki za Kibiashara almaarufu bodaboda katika manispaa
ya Shinyanga,kujiua kwa kujinyonga kwa kutumia waya wa simu chumbani kwake.
Tukio hilo la kushangaza limetokea
Jumamosi Juni 10,2017 majira ya saa nane mchana katika mtaa wa Mwinamila kata
ya Ngokolo katika manispaa ya Shinyanga.
Mashuhuda wa tukio hilo walisema Jacob
Paul ambaye ni mwenyeji wa mkoa wa Kigoma alifika nyumbani kwake majira
ya saa saba mchana akiwa amepakizwa kwenye pikipiki na mwendesha bodaboda
mwenzake huku akionekana kuwa mtu mwenye furaha kisha akaingia ndani kwake.
Walieleza kuwa baada ya takribani
dakika 30 watoto wawili marehemu walifika nyumbani wakitaka kuingia ndani ya
nyumba lakini mlango ulikuwa umefungwa kwa ndani walijaribu kumuita lakini
hakujibu ndipo wakaamua kwenda kuchungulia dirishani.
Walifafanua kuwa watoto hao
walipochungulia dirishani walimuona baba yao akiwa amening’inia chumbani kisha
kutoa taarifa kwa majirani na baba mwenye nyumba akaamua kutoa taarifa kwa
jeshi la polisi.
“Mke wa marehemu hakuwepo tulipoona kuwa mlango ni
mgumu kufunguka tuliamua kuuvunja na kumkuta amejiua na huenda chanzo cha kifo
chake kimetokana na msongo wa mawazo kwa sababu tangu kutokea kwa tukio la
mwendesha bodaboda Joel Gabriel Mamla (26) kufariki dunia,alikuwa anasema
waendesha bodaboda wenzake wamekuwa wakimlalamikia kuwa anashirikiana na polisi
kukamata waendesha bodaboda waliofanya vurugu hivi karibuni”,alieleza
jirani Sarah Edward.
“Jana alikuwa anasema kuwa anapewa vitisho na wenzie
kuwa anawasaliti na kusababisha waendesha wakamatwe na polisi na pikipiki zao”,alieleza
jirani huyo.
“Nilikwambia mme wangu ujiuzulu uenyekiti,ona sasa
waendesha bodaboda wenzako wamekuponza,wamekusababishe ujiue baba
Joshua,umeacha familia yako bora,watoto hawa watalelewa na nani”, alisikika mke
wa marehemu, Rebeca Amos aliyekuwa analia muda wote wakati wa tukio,akiomboleza
kwa uchungu.
Alisema mme wake amekuwa akipokea
vitisho kwa watu wasiojulikana wakimtuhumu kuwasaliti na kusababisha wakamatwe.
Habari kutoka eneo la tukio zinasema
kuwa marehemu alikuwa analalamikiwa na waendesha bodaboda wenzake kuwa
anashirikiana na jeshi la polisi kugandamiza waendesha bodaboda wenzake.
“Mwenyekiti anadaiwa kuwasaliti
wenzake,hata kipindi kile mwendesha bodaboda Boaz William aliyefariki dunia kwa
kugongwa gari wakati akidaiwa kuwakimbia askari wa usalama barabarani mjini
Shinyanga anadaiwa kushirikiana na polisi kutorosha mwili wa marehemu na
kuupeleka Kigoma kwa ajili ya mazishi ambapo hata waendesha bodaboda hawakupata
hata nafasi ya kuaga mwili wa marehemu”,ilielezwa Malunde1 blog.
Diwani wa kata ya Ngokolo,Emmanuel
Ntobi alifika eneo la tukio alimuomba rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Dkt. John Pombe Magufuli kuunda tume huru ya kijaji kuchunguza vifo vya
waendesha bodaboda katika manispaa ya Shinyanga.
“Sasa idadi ya vifo
vya waendesha bodaboda vimetokea Shinyanga,kuna utata kwani jamii inasema vifo
vinasababishwa na askari polisi huku jeshi la polisi nalo likidai waendesha
bodaboda ndiyo wanasababisha vifo vyao kwa kukiuka sheria za usalama
barabarani,mpaka sasa pikipiki nyingi zimekamatwa”,alieleza
Ntobi.
Kamanda wa jeshi la polisi ACP Muliro
Jumanne Muliro aliyekuwepo eneo la tukio alisema wamekuta mwenyekiti huyo wa
waendesha bodaboda amejinyonga kwa kutumia waya mgumu wa simu katika chumba
chake.
“Tumepata taarifa kuhusu tukio
hili,tulipofika tumekuta amefariki kwa kujing’iniza kwa waya,tumeuchua mwili wa
marehemu kwa ajili ya kuufanyia uchunguzi hospitalini,sisi kazi yetu ni
kuchunguza chanzo cha kifo,bado tunafanya uchunguzi zaidi juu ya tukio hili
tutatoa taarifa zaidi baadaye”,alisema kamanda Muliro.
Tukio la mwenyekiti wa waendesha
bodaboda kujiua limetokea siku tano tu baada ya jeshi la polisi mkoani
Shinyanga,kulazimika kuwapiga mabomu ya machozi waendesha bodaboda, kwa kitendo
cha kuundamana kupinga kifo cha mwenzao Joel Gabriel Mamla (26),kilichodaiwa
kusababishwa na askari polisi PC Edmund baada ya kumkamata kwa kosa la kutovaa
helmet. SOMA <<HAPA>>
Kwa mujibu wa jeshi la polisi watu 26
walifikishwa katika mahakama ya wilaya ya Shinyanga kwa mashtaka ya kufanya
mkusanyiko usio halali,kufanya fujo na kujaribu kufanya maandamano kinyume na
sheria.
Kati yao David Laurent alikiri kosa
lake na kuhukumiwa kifungo cha miezi sita jela na wengine kesi yao iliahirishwa
na itaendelea Julai 23,2017.