MFUMUKO wa Bei wa Taifa kwa mwezi Mei, 2017 umepungua kwa asilimia 0.3,kutoka ule wa Mwezi April mwaka huu.
Mfumuko huo kwa bei ya Taifa,umepungua hadi kufikia asilimia 6.1 kutoka asilimia 6.4 ilivyokuwa mwezi Aprili, 2017.
Akizungumza
na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam leo Mkurugenzi wa Sensa ya
Watu na Takwimu za Jamii, Ephraim Kwesigabo amesema kupungua kwa mfumuko
wa bei kunatokana na kupungua kwa kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na
huduma ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo kwa mwezi Aprili, 2017.
“Mfumuko
wa Bei wa Taifa umepungua kutoka asilimia 6.4 kwa mwezi Aprili, 2017
hadi kufikia asilimia 6.1 kwa mwezi Mei , 2017 kutokana na kupungua kwa
kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Mei, 2017,”
amesema Kwesigabo.
Kwesigabo
amesema Mfumuko wa Bei wa mwezi Mei, 2017 unaopimwa kwa kipimo cha
mwezi umeongezeka kwa asilimia 0.2 ikilinganishwa na ongezeko la
asilimia 0.5 ilivyokuwa mwezi Aprili, 2017.
Amesema
Fahirisi za Bei zimeongezeka hadi 109.26 kwa mwezi Mei, 2017 kutoka
109.04 mwezi Aprili, 2017 kutokana na kuongezeka kwa bei za baadhi ya
bidhaa za vyakula na zisizo za vyakula.
Kwesigabo
ametaja bidhaa za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa fahirisi kuwa ni
pamoja na mahindi yaliyoongezeka kwa asilimia 4.2, maharage mabichi kwa
asilimia 2.9, maharage ya soya kwa asilimia 2.2, unga wa mtama kwa
asilimia 1.5, viazi mviringo kwa asilimia 2.0, mihogo mikavu kwa
asilimia 2.3, na magimbi kwa asilimia 2.5.
Aidha bidhaa zisizo za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa fahirisi za bei ni pamoja na mkaa ulioongezeka kwa asilimia 2.5.
Ameongeza
kuwa Mfumuko wa Bei kwa bidhaa za vyakula nyumbani na migahawani kwa
mwezi Mei, 2017 umepungua hadi asilimia 11.8 kutoka asilimia 12.0 mwezi
Aprili, 2017. Aidha, badiliko la Fahirisi za Bei kwa bidhaa zisizo za
vyakula umepungua hadi asilimia 3.0 mwezi Mei, 2017 kutoka asilimia 3.4
mwezi Aprili, 2017.
KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI