RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania,John Magufuli, Jumatatu anatarajia kukabidhiwa taarifa ya kamati ya pili ya wachumi na
wanasheria iliyofanya uchunguzi wa mchanga wa dhahabu ( Makinikia ) uliokuwa
katika makontena 227,yanayomilikiwa na Kampuni ya Madini ya Acacia.
Mchanga huo wa madini uliokuwa kwenye
makontena,ulizuiliwa kusafirishwa nje ya nchi kama ilivyokuwa ada yake,na
kuundiwa tume mbili,ambapo Kamati ya awali iliishakabidhi Ripoti yake,na
kubakiwa na ile ya pili,ambayo nayo tayari imeshakamilisha majukumu yake,na
kuwa tayari kuikabidhi kwa Rais Magufuli.
Taarifa iliyotolewa leo (Jumamosi) na
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa imesema tukio hilo
litarushwa hewani moja kwa moja kupitia redio, televisheni, mitandao ya kijamii
na tovuti rasmi ya Ikulu ambayo ni www.ikulu.go.tz kuanzia saa 3:30 asubuhi.
Ikulu imewakaribisha wananchi
kufuatilia matangazo hayo kupitia vyombo hivyo au simu za mkononi kwa
kutembelea tovuti hiyo.
Mei 24, Rais Magufuli alipokea ripoti
ya kamati ya kwanza yenye wajumbe wanane iliyochunguza aina na viwango vya
madini yaliyomo kwenye mchanga wa madini uliomo ndani ya makontena
yaliyozuiliwa na Serikali kusafirishwa nje ya nchi.
Kamati hiyo aliiteua Machi 29, mwaka
huu ikiwa na wajumbe ambao ni wana taaluma katika fani za jiolojia, kemia,
uhandisi kemikali na uhandisi uchenjuaji madini.
Baada ya kuipokea ripoti hiyo, Rais
Magufuli alitengua uteuzi wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter
Muhongo.
Rais Magufuli pia aliivunja Bodi ya
Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) na kumsimamisha kazi mkurugenzi
mtendaji wake.