Tuesday, May 2, 2017

LUGHA CHAFU KWA WAGONJWA,KIKWAZO KUJIUNGA CHF.

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO



   
IMEELEZWA jitihada za Halmashauri ya Msalala,wilayani Kahama,kuhamasisha wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF),zinakwazwa na
kauli mbaya zitolewazo na Wauguzi.

Watumishi hao wa Idara ya Afya,wamekuwa na lugha zisizo rafiki kwa wanaowahudumia,kiasi cha kuwakatisha tamaa wagonjwa wanaofika katika vituo vya Afya kwa lengo la kupatiwa matibabu.

Diwani wa viti maalumu Kata ya Segese,Angela Paul,ameyabainisha hayo katika Kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika juzi mjini Kahama,kwa kuwataka watumishi wa Idara ya Afya,wajirekebishe na kuondokana na lugha chafu kwa wagonjwa ili jamii ihamashike kujiunga na CHF.

Diwani huyo alisema kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi wanaofika katika zahanati na vituo vya afya,vilivyo Halmashauri ya Msalala, kuwa watumishi wa idara hiyo wamekuwa wakiwajibu wagonjwa majibu ya kukatisha tamaa pindi wanapoenda kupatiwa huduma za afya.

“…huu mpango wa CHF,utawawia vigumu kuenea katika vijiji vyetu pindi lugha chafu kutoka kwa Wauguzi wetu haitokoma,kwani wamekuwa na vitisho na majibu machafu yanayokatisha tamaa yanayotolewa na watumishi hao,hivyo jamii kupata hofu kwenda kupata matibabu.” Alisema Angela.

Angela alidai kuwa tatizo kubwa la lugha chafu zinazotolewa kwa wagonjwa na watumishi hao ni kutokana na watumishi hao kufanya kazi kwa mazoea huku asilimia kubwa ya watumishi hao wamedumu katika vituo vyao vya kazi kwa muda mrefu.

Aidha diwani huyo hakusita kulaumu mfuko huo wa afya ya jamii(CHF) kwani pamoja na wananchi vijijini kuchangia mfuko huo lakini changamoto kubwa imekuwa ni kukosekana kwa dawa katika vituo vya afya pamoja na zahanati zilizopo katika maeneo yao.

Alisema kuwa amekuwa akifanya ziara nyingi vijijini za kuhamasisha wananchi kujiunga na mfuko huo ambapo wamekuwa na mwitikio mkubwa lakini changamoto kubwa aliyoiona ni kukosekana kwa dawa jambo ambalo linawakatisha tamaa wananchi walio wengi kujiunga na mfuko huo. 

Naye Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Msalala,Dr. Hamad Nyembea, aliliambia baraza hilo kuwa upatikanaji wa dawa hivi sasa ni mzuri kwa kipindi cha miaka mitatu na kuongeza kuwa  dawa muhimu zinapatikana katika vituo vyote kwa asilimia 75.

Akizungumzia kwa kutolewa kwa Lugha chafu kwa wagonjwa Nyembea alikiri kuwa tatizo hilo lipo na kuongeza kuwa tatizo hilo linashughulikiwa na mpaka sasa malalamiko mengi yalionyesha kupungua katika maeneo mengi,huku akibainisha kuwepo kwa mkakati wa kuwabadiri vituo vya kazi kwa watumishi waliohudumu eneo moja kwa kipindi kirefu .

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo,Simon Berege,aliwaonya watumishi wanaoendelea kutoa lugha chafu kwa wagonjwa na kuahidi kulitafutia ufumbuzi suala hilo na kudai kuwa iwapo atabainika mtumishi yoyote wa afya kukutwa na kosa hilo halmashauri haitasita kumchukulia hatua za kinidhamu.

“Niwaombe wananchi wa Msalala kutosita kutoa taarifa kwa viongozi,pindi watakapobaini kuna mtumishi wa idara hii bado anaendelea kutoa lugha chafu kwa wagonjwa,nami sitasita kuchukua hatua kali dhidi yake kwani tulishaelekezana kupitia vikao vyetu vya utumishi,” Alisema Berege.



KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI