Tuesday, March 21, 2017

KIGOGO HALMASHAURI ASIMAMISHWA KAZI

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO



HALMASHAURI ya Mji wa Kahama imemsimamisha Kazi,Mkuu wa Idara ya Ardhi na Maliasili,Joachim Henjewele,huku ikiwataka watumishi wengine watatu
katika Idara hiyo kujieleza kutokana na tuhuma zinazowakabili juu ya kukithiri kwa migogoro ya Ardhi Mjini Kahama.


Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kahama,Anderson Msumba,alisema Henjewele alisimamishwa kazi kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazomkabili za kushindwa kuwajibika ipasavyo kwenye idara hiyo na kuwa chanzo cha migogoro ya Ardhi. 

Msumba alisema mbali na Halmashauri kumsimamisha Mkuu huyo wa idara pia imewaandikia barua ya kujieleza kwanini wasichukuliwe hatua,maafisa watatu katika Idara hiyo ambao ni Ofisa Mipango Miji; Irene Maro,Ofisa ardhi mpimaji Yahaya Msangi na afisa ardhi katika halmashauri hiyo,Yusuph Luhumba.

Maamuzi hayo ya Halmashauri yamechukuliwa kufuatia  Kamati ya Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkurlu,iliyoundwa mwishoni mwa mwaka jana na kuongozwa na Ofisa Tawala wake;Said Yasini,kuchunguza migogoro ya ardhi kwenye Halmashauri ya Mji wa Kahama,kubaini ukiukwaji mkubwa katika suala la upimaji wa viwanja kwenye maeneo mbalimbali ya mji huo .

Kufuatia ripoti hiyo,Mkuu wa Wilaya ya Kahama,alitoa agizo katika Baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo,kuwachukulia hatua watumishi wote waliohusika kuvuruga upimaji wa viwanja hivyo ikiwa ni pamoja na kufanya uchunguzi kwenye makampuni yaliyokuwa yakihusika na zabuni ya upimaji wa viwanja hivyo.

Hata hivyo Henjewele,ambaye yupo likizo alipoongea na mwandishi wa habari hii alipingana na Mkurugenzi wake kwamba amesimamishwa kazi,bali alikiri kupokea barua ya kujieleza aliyoipata akiwa mapumzikoni.

Kwa upande wa Umoja wa Wazee wa wilaya ya Kahama (UWAKA),umedai kutoridhishwa na hatua hizo zilizochukuliwa kwa watu wachache huku idara nzima ikiwa haiwajibiki ipasavyo na kusababisha kuibuka kwa mogogoro ya viwanja mara kwa mara..

Katibu UWAKA, Paul Ntelya,alisema umoja huo unaona hatua zilizochukuliwa pamoja na kuwakumba baadhi ya vigogo katika Idara ya Ardhi,lakini hazijagusa vinara wa migogoro,ambao  baadhi yao wakisalimika pasipo hata kupewa onyo huku wakihusika na kuuza maeneo mengi,mjini Kahama,likiwemo la Nyahanga.

“Tunajiuliza kwanini aliyehusika kuuza eneo Nyahanga ambalo limejengwa maghala licha ya mmiliki wake kuzuiwa,kwakuwa ni eneo la Shule ya Msingi Nyahanga,lakini pamejengwa,na aliyehusika kuuza eneo hilo wakishindwa kumchukulia hatua,”alisema Ntelya.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI