KAMATI ya pili iliyoundwa na Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.John Pombe Magufuli,kuchunguza mchanga wa
dhahabu unaosafirishwa nje ya nchi,imewasilisha Taarifa yake kwa
kubainisha
kilichosafirishwa si mchanga bali ni madini anuai.
Kamati hiyo iliyokuwa na wabobezi wa
masuala ya Uchumi na Sheria,pia imebaini kuwa kampuni ya ACACIA Mining Plc inayojishughulisha
na uchimbaji na kusafirisha kilichoelezwa Mchanga wa dhahabu ( Makinikia )haina
kibali na inafanya kazi kinyume cha sheria.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo,Profesa
Nehemiah Osoro akiwasilisha taarifa yao,amesema Kamati yake imebaini kuwa kilichokuwa
kikisafirishwa na Acacia,hakikuwa mchanga wa dhahabu,bali ni mkusanyiko wa
madini zaidi ya kumi ambayo yangeliingizia Taifa pato.
Profesa Osoro amesema pia Kamati yake
imebaini kwamba Kampuni hiyo ya Acacia haina uhalali wa kufanya shughuli zake
hapa nchini na imetenda makosa yakiwemo kujipatia mali kwa udanganyifu,
uhujumu uchumi, jinai na kuitia hasara taifa.
Aidha Kamati ya Prof. Osoro imebaini
kwamba Makinikia yaliyouzwa nje ya nchi hayakuwa makinikia hasa, bali
yalikuwa ni madini mbalimbali huku ikiongeza kwamba katika mikataba ya
uuzwaji wa makinikia hayo, serikali haikuwa sehemu ya mikataba hiyo.
Prof. Osoro ameongeza kwamba jumla ya
mapato yote ambayo serikali imepoteza ni Tsh. trilion 68.6 sawa na bajeti ya
miaka miwili ya nchi kodi ya mapato ambayo taifa imepoteza ni Tsh. tril 55.07,
mrahaba tril 11, bandari tril 1.6. na kwamba jumla ya thamani ya madini kwenye
makontena yote 44,277 tangu mwaka 1998 ni Tsh. tril 132.56.
Pamoja na hayo imebainika kuwa
uongezwaji wa leseni kinyume cha sheria ambapo imedaiwa kuwa aliyekuwa Waziri
wa Nishati na Madini William Ngeleja na Sospeter Muhongo ndio waliohusika
na uongezaji wa muda kwenye uchimbaji wa madini.
Kamati hiyo imetoa mapendekezo Ishirini
ambayo Rais Magufuli ameyaridhia ikiwepo kuchukua sheria juu ya kampuni ya
ACACIA iliyopo nchini kinyume cha sheria kupitia msajili wa makampuni,sambamba
na sheria za madini kuwasilishwa Bungeni na kujadiliwa.
Pia Mawaziri na watendaji wote wa
serikali walioshiriki kwa namna moja au nyingine juu ya mikataba ya uchimbaji
madini,wachukuliwe hatua za kisheria huku ikiitaka Serikali iwe inafanya
ukaguzi wa mara kwa mara kwenye makampuni ya madini.