Wednesday, April 19, 2017

WANAKIJIJI WALALAMIKA SHINIKIZO LA KODI WANALOTOZWA NA HALMASHAURI

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO




WANANCHI wa Kata ya Lunguya katika Halmashauri ya Msalala,Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga,wamelalamikia tozo za Ushuru mbalilmbali wanazoshinikizwa  kulipa na maafisa wa biashara katika
Halmashauri yao.

HIvyo wamemuomba mbunge wa Jimbo hilo, Ezekiel Maige,awasaidie kutatua kero hiyo ambayo inawadhoofisha kiuchumi kutokana na kulazimika kulipa ushuru  usiozingatia mfanyabiashara mdogo ama mkubwa,anaandika Michael Francis Bundala. 

Wakizungumza mara baada ya mbunge huyo kutembelea katika kitongoji cha Nyangarata,Vijiji vya Kalole na Kabanda, wamemuomba mbunge huyo kuchukua hatua za makusudi ili aweze kuwasaidia.

Wamesema licha ya Rais Magufuli kukataza ushuru kwa wafanyabiashara wadogo lakini halimashauri hiyo inaendelea kutoza ushuru kwa wafanyabiashara wadogo na mama lishe na bila kuzingatia kiwango cha mtaji cha kila mfanyabiashara au mama lishe.

Hilda Julius mkazi wa Kata ya Lunguya,amehoji vipi mchuuzi wa mchicha unaotembezwa katika beseni atozwe kodi ya Shilingi Elfu Kumi na tano kwa mwezi,ilhali kipindi cha Kampeni Rais John Magufuli,alinadi ilani ya CCM kwa kueleza kutotozwa kodi ndogo ndogo?

Nae Nae Petro Shaba Madiba anasema hawapingi kulipa ushuru kwakuwa wanatambua ni wajibu wao lakini wanachokipinga ni kutozwa ushuru mkubwa usiolingana na kipato chao ama ukubwa wa biashara,huku wakilazimika kulipa kiwango kinacholingana na wenye biashara kubwa jambo analodai ni kuwaumiza wafanyabiashara wadogo.

Kufuatia malalamiko hayo Mbunge wa Jimbo la Msalala,Ezekiel Maige, amewaahidi wananchi hao kulishughulikia suala hilo mapema iwezekanavyo kwa kuwa linakiuka kile kilichozungumzwa na Rais wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka 2015.

“…ushuru umebaki kwa wafanyabiashara wanaosafirisha mazao na si kwa wanaouza ili wajikimu kimaisha,boda boda na wauza mchicha ushuru umekatazwa kwa mujibu wa maelekezo ya Rais Magufuli,lakini hapa kuna mkanganyiko,hivyo ntalishughulikia na mtaletewa  muongozo kamili na Halmashauri unaofafanua hayo maelekezo ya Rais.”Anasema Maige.

Kwa upande wake Diwani wa Kata hiyo,Benedict Manuali,amesema suala la ushuru limekuwa na mkanganyiko mkubwa katika kata hiyo ambapo wananchi wa eneo hilo wamekuwa wakilalamika kutozwa ushuru ambao hauangalii mtaji wa mfanyabiashara.

Manuali anasema,“malalamiko hayo pia aliwahi kuyapata toka kijiji cha Kalole,ambapo mama lishe,wauza mbogamboga wanakumbana na kero hiyo,niliiwasilisha kwa Mkurugenzi ambaye aliahidi kutuma wataalamu kuja kuwaelimisha ikiwemo matumizi ya mashine za kietroniki za kutozea kodi,lakini hakuna lililofanyika.”

Katika hatua nyingine Mbunge wa jimbo hilo ametoa mifuko 100 ya saruji katika kitongoji cha Nyangarata kwa kuwa wananchi wa eneo hilo wamekubaliana kujenga shule kwa nguvu zao wenyewe ili watoto wao wapate shule na waepukane na suala la watoto wao kusafiri umbali mrefu kwenda kusoma.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI