Thursday, April 20, 2017

RAIS MAGUFULI APONGEZWA KUZUIA MCHANGA WA MADINI KUSAFIRISHWA NJE

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO



KITENDO cha Serikali ya awamu ya tano,kuzuia Mchanga kutoka eneo la
madini,kusafirishwa nje ya nchi,kimepongezwa kuwa cha Kizalendo,kilichopaswa kudhibitiwa kipindi kirefu.

Maamuzi hayo yanastahili kuungwa mkono kwakuwa yanaokoa rasilimali,iliyosafirishwa nje ya nchi kwa kumnufaisha Mwekezaji pasipo kuwa na tija kwa Taifa la Tanzania,anaandika Michael Francis Bundala.
                                                
Baadhi ya Wananchi wa kijiji cha Kakola,Kata ya Bulyanhulu katika Halmashauri ya Msalala,wilayani Kahama,wamefurahishwa na maamuzi hayo na kudai wapo tayari kuandamana mwendo mrefu  kuunga mkono juhudi za Rais wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dk John Pombe Magufuli za kuzuia mchanga kusafirishwa nje ya nchi.

Shauku yao hiyo wameileza katika mkutano wa hadhara,walipotembelewa na Mbunge wa Jimbo  la Msalala,Ezekiel Maige,kusikiliza kero zao,ambapo walimpongeza Rais Magufuli kwa madai amefanya jambo muhimu walilokuwa wakilisubiri.

Wakieleza kero zao kwa mbunge huyo wamesema wamechoshwa na unyonyaji unaofanywa na mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu,unaomilikiwa na Kampuni ya ACACIA,uliopo katika kata yao,umekuwa ukitoa ahadi za kusaidia maendeleo kisha  baadaye  kushindwa kutekeleza,hivyo kuzuia mchanga kusafirishwa nje ni hatua nzuri iliyofanywa na Rais.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kakola,Emmanuel Bombeda,amesema usafirishaji mchanga huo umenufaisha baadhi ya watumishi mgodini,ambao ni Watanzania ambao hawana mioyo ya kizalendo zaidi ya kuangalia maslahi yao binafsi.

Anasema,“ tunaunga mkono kwa Rais Magufuli kuzuia wizi huo,kwani tunaushahidi wa asilimia 99 watu hao ni wezi kwa kusafirisha mchanga huo ambao ungelibaki ungelinufaisha wachimbaji wadogo wadogo wanaopatikana katika kijiji cha Kakola.”

Mkazi wa Kijiji cha Kakola,Albert Wakati Sagembe,amesema tatizo kubwa la Mgodi huo kutokuwa na Meneja Uhusiano kutoka Kanda ya Ziwa,ambaye angelikuwa na uchungu kwa kuhakikisha anasimamia maendeleo stahiki ya eneo lililo pembezoni na Mwekezaji.

Mbunge wa jimbo hilo, Ezekiel Maige amesema yupo pamoja na wananchi hao na watakapotaka kuandamana atashirikiana nao  kuomba kibali cha kufanya maandamano ya amani kwa kuwa Mgodi huo wa Bulyanhulu umekuwa hautekelezi majukumu yake kwa wananchi.

“….walituahidi kutuboreshea miundo mbinu ya barabara huduma za jamii hapa Kakola kama afya,elimu na maji,ambayo haijatekelezeka,kwa ujumla hawana mkakati mzuri wa kusaidia maendeleo jambo ambalo wameonesha si waungwana,kwa kuahidi pasipo kutimiza.”Anasema Maige.

Aidha Mwenyekiti wa kijiji hicho,Bombeda  amemshukuru mbunge huyo kwa kufika katika eneo hilo kusikiliza kero za wananchi na kumuomba mbunge huyo kuyafanyia kazi malalaniko ya wananchi kuhusu  mgodi wa Bulyanhulu.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI