Monday, April 17, 2017

MIGOGORO YA ARDHI CHANZO CHAKE WATUMISHI WA MUDA MREFU KAZINI

BOFYA HAPA CHINI KUONA MAAJABU YA LEO



WATUMISHI wa Kitengo cha Ardhi na Mipango Mji katika Halmashauri ya Mji wa Kahama,ambao wamehudumu kwa kipindi kirefu,wametakiwa kuhama kutokana na kubainika kuwa
ndio chanzo cha kukithiri kwa migogoro ya Ardhi.

Imedaiwa utumishi wao kwa kipindi kirefu,katika Halmashauri ya Mji wa Kahama,kumewapa ujasiri wa kutekeleza majukumu yao kwa maslahi binafsi pasipo kujali wanazalisha migogoro ya Ardhi inayokosa utatuzi,ambayo imekuwa kero kwa wakazi wa Kahama.

Tuhuma hizo zimebainishwa katika Kikao kawaida cha Baraza la Madiwani  wa Kahama kilichokaa kwa lengo la kujadili taarifa ya robo ya tatu ya shughuli za utekelezaji za Halmashauri hiyo  zilizofanyika katika kipindi hicho,huku likitolewa pendekezo la kuhamisha watumishi hao ambao wamekuwa hawana tija katika Halmashauri hiyo.

Katika Kikao hicho,Madiwani walimshauri Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Kahama,kufanya mchakato wa kuiomba Tamisemi kuwahamisha watumishi hao,kutokana na kuhudumu kwa kipindi kirefu katika Mji wa Kahama,huku wakisababisha kuongezeka kwa migogoro ya ardhi katika Mji huo.

“Kwa nini hawa watumishi wa Idara ya Ardhi na Mipango Miji  wasibadilishane na wale wa Shinyanga, Washinyanga waje Kahama na hawa wa Kahama waende Shinyanga kwani kunashindikana nini? Hawa wamekaa muda Mrefu hapa na ndio wanaosababisha migogoro isiyoisha ya ardhi hapa Mjini”, Alihoji Diwani wa Viti Maalumu,Kata ya Kahama Mjini,Aoko Nyangusu.

Madiwani hao walimtaka Mkurugenzi wa Halmashauri  hiyo kuhakikisha anakamilisha mchakato wa kuwakataa na kuwahamisha watumishi hao mapema iwezekanavyo,kinyume cha hapo wametishia kufikia maazimio ya kumkataa Mkurugenzi huo,hali ambayo italeta mkanganyiko mkubwa katika Halmashauri hiyo ya Mji.

Aidha Diwani huyo aliomba kama kuna kanuni inayomzuia Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji kuhudhuria vikaao vya Kamati ya Ardhi na Mipango Mji,itenguliwe ili apate fursa ya kuhudhuria,hatua itakayosaidia kutatua kwa haraka migogoro hiyo ya ardhi ambayo imekuwa changamoto kubwa ya Maendeleo katika Mji wa Kahama.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kahama Abel Shija alisema kuwa kwa  sasa Halmashauri yake imejitahidi kwa kiasi kikubwa kutatua migogoro ya ardhi iliyokuwepo hapo  zamani na kuongeza kuwa kwa sasa hali imekuwa tofauti kwani migogoro imepungua kwa kiasi fulani kwa Wananchi.

“Kwa sasa migogoro ya ardhi iliyokuwepo hapo zamani imepungua kwa kiwango kikubwa,hapo awali Maafisa ardhi walikuwa wakigawa kiwanja kimoja kwa watu karibuni saba na kuleta mvutano huku Halmashauri ikipata lawama kubwa kutoka kwa Wananchi wa mji wa Kahama,sasa hali hiyo haipo”. Alisema Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Kahama.

Nae Katibu Tawala wa Wilaya ya Kahama  Timoth Ndanya alisema kuwa Migogoro ya ardhi katika Mji wa Kahama ni mingi  na kuwataka madiwani na watumishi wa Halmashauri hiyo kushirikiana kuitatua huku wakihakikisha haizaliwi migogoro mingine.

Kikao hicho cha Baraza la Madiwani kiliamua kuunda Kamati ya kuchunguza na kufuatilia migogoro ya ardhi katika Halmashauri hiyo,pamoja na maeneo ya makaburi yaliyovamiwa kujengwa nyumba za makazi,ikiwa ni kamati ya pili kuundwa kwani awali  Mkuu wa Wilaya ya Kahama alishaunda Kamati kwa ajili ya kufuatilia suala hilo.

KUONA VIDEO MPYA BOFYA HAPA CHINI